Kati ya Vita na Amani: Afrika Iliyonaswa Kati ya Machafuko ya Mikataba ya Kusitisha Mapigano na Migogoro ya Njia za Baharini na Biashara

Na Rami Zuhdi — Makamu Rais wa Kituo cha Kiarabu cha Utafiti na Mafunzo ya Kimkakati
Bara la Afrika katika wakati huu wa sasa linaonekana kana kwamba limesimama ukingoni mwa jiografia iliyovurugika, ambapo ramani za vita zinatofautiana na ramani za biashara, katika hali hii, mahesabu ya uhuru wa nchi yanakinzana na mantiki ya njia za kimataifa zilizowazi na zilizofungwa. Vita barani Afrika siyo tena migogoro ya ndani ya kimila; Badala yake, vimegeuka hatua kwa hatua kuwa vipengele vinavyochangia kupanga upya njia za biashara duniani na kuwa zana za shinikizo zisizo za moja kwa moja kwenye mnyororo wa usambazaji wa kimataifa, hasa kutokana na kuongezeka kwa utegemezi wa dunia wa njia za baharini zinazozunguka bara hili kutoka Mashariki, Magharibi, na Kaskazini.
Kuanzia Sudan hadi ukanda wa Sahel, na kutoka Pembe ya Afrika hadi Libya, aina za migogoro ni nyingi lakini matokeo yake yanakaribia kufanana: Kudhoofisha mataifa, kusambaratika kwa mfumo wa kiuchumi, na kuongezeka kwa udhaifu wa njia za nchi kavu na baharini. Vita vya Sudan pekee, ambavyo vimeingia mwaka wake wa nne huku kukiwa na mporomoko mkubwa wa kibinadamu, vimesababisha mamilioni ya watu kuyahama makazi yao na kushuka kwa kasi kwa uzalishaji wa kilimo na viwanda. Makadirio ya kimataifa yanaonyesha kuwa uchumi wa Sudan umepoteza zaidi ya 40% ya uwezo wake halisi wa uzalishaji tangu kuanza kwa mgogoro huo. Hizi si namba tu, bali ni viashiria vya nchi inayovunjwa mbele ya macho ya eneo lenye msukosuko.

Wakati huo huo, Bahari Nyekundu inasalia kuwa moja ya njia muhimu zaidi za biashara duniani, ambapo takriban 10% hadi 12% ya biashara ya kimataifa hupita hapo, na karibu 30% ya harakati za makontena duniani zinazohusiana na nishati na bidhaa za kimkakati. Huku kukiwa na kuongezeka kwa mvutano katika mlango wa Bab al-Mandab na Pembe ya Afrika, njia za baharini zimegeuka kutoka kuwa mishipa ya kiuchumi na kuwa sehemu zenye udhaifu wa kimkakati. Usumbufu wowote wa kiusalama au kijeshi unaweza kubadilisha mwelekeo wa biashara kuelekea njia ndefu na zisizo na ufanisi, jambo ambalo litaleta gharama kubwa ya kiuchumi duniani.
Mwingiliano huu kati ya vita na njia za biashara si wa bahati mbaya; unaonyesha mabadiliko ya kimfumo katika asili ya migogoro ndani ya bara la Afrika. Mataifa ya kikanda na kimataifa sasa yanatambua kuwa udhibiti wa maeneo yenye ushawishi haupatikani tu kupitia ardhi, bali kupitia udhibiti wa vituo vya baharini na milango ya biashara. Hii inaelezea ushindani unaoongezeka wa bandari za Afrika, vituo vya usambazaji wa kijeshi baharini, na maeneo ya ushawishi wa kilojistiki kuanzia Bahari ya Hindi hadi Mediterania.
Kwa upande mwingine, Afrika inaonekana katika sehemu nyingi kana kwamba inaishi katika hali ya kusitisha mapigano kwa muda, ambapo vita husimama bila kumalizika, njia hufunguliwa bila kutulia, na mikataba husainiwa bila kutekelezwa kikamilifu. Hali hii “ya kijivu” inatengeneza uchumi dhaifu—uchumi ambao haupo kwenye hali ya vita kamili wala katika hali ya amani endelevu, bali upo katikati ambapo rasilimali zinapotea na hasara zinaendelea kuongezeka kimyakimya.
Pia, inashangaza kuwa uamuzi wa kufungua au kufunga njia za baharini na biashara si uamuzi wa mamlaka kamili ya nchi za Afrika tena, badala yake, umekuwa ukihusiana na mtandao tata wa mizani ya kimataifa, ambapo maslahi ya mataifa makubwa yanaingiliana na mahesabu ya watendaji wa kikanda, hali hii inazalisha tena dhana ya “mamlaka pungufu” juu ya jiografia ya kiuchumi ya bara hili.

Kwa hali hii, pengo la maendeleo ndani ya Afrika linazidi kupanuka. Ripoti za Benki ya Dunia zinaonyesha kuwa bara hili hupoteza mabilioni ya dola kila mwaka kutokana na migogoro ya silaha, iwe kupitia kuvurugika kwa biashara, uharibifu wa miundombinu, au kuongezeka kwa gharama za bima na usafirishaji. Aidha, zaidi ya nchi 30 za Afrika bado zinakabiliwa na viwango tofauti vya udhaifu wa kisiasa na kiusalama, jambo linalofanya utulivu wa bara hili kuwa lengo linalochelewa kufikiwa badala ya kuwa uhalisia uliopo.
Afrika ya leo haijapotea kijiografia, lakini imepotea katika hali tata kati ya vita na amani, kati ya uwazi na ufungaji, kati ya njia zinazofunguliwa wakati mmoja na kufungwa wakati mwingine, na kati ya utashi wa maendeleo unaogongana daima na uhalisia wa mgogoro. Katika moyo wa hali hii, kuna hitaji la haraka la kufafanua upya usalama wa Afrika—si tu kama usalama wa kijeshi, bali kama usalama wa kiuchumi, kibiashara, na wa njia za usafirishaji.
Mustakabali wa bara hili hautaamuliwa tu katika medani za vita, bali katika uwezo wa kugeuza jiografia kutoka uwanja wa mapambano hadi kuwa jukwaa la kupitisha bidhaa, kutoka njia zinazopiganiwa hadi kuwa mishipa ya ushirikiano, na kutoka kwa kusitisha mapigano kwa muda hadi amani endelevu inayochora upya nafasi ya Afrika katika mfumo mpya wa ulimwengu ujao.



