Alarab Language

Mtazamo wa Kistratejia wa Nafasi ya Misri Katika Kupambana na Msimamo Mkali

Rami Zuhdi – Mtaalamu wa Masuala ya Afrika

Katika karne ya 21, janga la msimamo mkali si tatizo la kiusalama tu au changamoto ya ndani inayohusu nchi moja pekee, bali limekuwa miongoni mwa vitisho hatari zaidi vinavyovuka mipaka. Hii ni kutokana na uwezo wake wa kutumia nafasi ya mtandao, migogoro ya kiuchumi, udhaifu wa kisiasa, na migogoro ya silaha ili kuwaunga watu na makundi yao, kusambaratisha jamii, na kudhoofisha mataifa.

Katikati ya mazingira haya ya kikanda yaliyojaa machafuko, Misri inajitokeza kama miongoni mwa nchi muhimu zaidi zilizokusanya uzoefu wa kivitendo, kifikra, na kitaasisi katika kupambana na ugaidi na msimamo mkali. Hili halikufanyika kwa njia ya ukali wa kiusalama pekee, bali kupitia ujenzi wa mfano jumuishi unaounganisha maendeleo, kurekebisha mitazamo ya kidini, na kuimarisha taasisi za taifa.

Uzoefu wa Misri umethibitisha kuwa kabiliano la kiusalama, ingawa ni muhimu, halitoshi peke yake kutokomeza msimamo mkali. Makundi ya kigaidi yana uwezo wa kujirudia kama mazingira yanayostawisha fikra kali yataendelea kuwepo. Ndiyo maana nchi ya Misri ilihamia kwenye dhana pana zaidi inayojikita katika kutatua vyanzo vikuu vinavyoruhusu kuenea kwa msimamo mkali, viwe ni vya kiuchumi, kijamii, kifikra, au kuelimu.

Mtazamo huu wa kistratejia unaenda sambamba na mabadiliko yanayotokea duniani, ambapo Umoja wa Mataifa unasisitiza kuwa ugaidi hauwezi kutenganishwa na changamoto za maendeleo, udhaifu wa taasisi za nchi, na migogoro ya muda mrefu. Kadhalika, ripoti za kimataifa zinaonyesha kuwa bara la Afrika limekuwa moja ya maeneo yaliyoathirika zaidi na ugaidi duniani, kwani katika miaka ya hivi karibuni lilishuhudia zaidi ya nusu ya waathirika wa mashambulizi ya kigaidi duniani kote, hususan katika eneo la Sahel na Pembe ya Afrika. Jambo hili linaongeza mara dufu umuhimu wa nafasi ya Misri ndani ya eneo lake la Afrika.

Nguvu halisi ya mfano wa Misri inategemea njia tano zinazokwenda sambamba:

  • Kwanza:Kulinda taifa na kudumisha taasisi zake kama safu ya kwanza ya ulinzi dhidi ya machafuko.
  • Pili:Maendeleo ya kiuchumi kama silaha endelevu zaidi ya kukausha vyanzo vya msimamo mkali, kwani uzoefu umethibitisha kuwa ukosefu wa ajira, umaskini, na kutengwa ni mazingira yenye rutuba kwa vijana.
  • Tatu:Kabiliano la kifikra kupitia taasisi za kidini zenye msimamo wa wastani, zikiongozwa na Al-Azhar Al-Sharif na Dar Al-Ifta ya Misri, ambazo zimekuwa marejeo ya kimataifa katika kueneza fikra za wastani na kupinga kauli za makundi yenye msimamo mkali.
  • Nne:Kuboresha elimu, utamaduni, na vyombo vya habari ili kuimarisha maadili ya uraia, uzalendo, na utofauti.
  • Tano:Kuendeleza uwezo wa kiusalama, kijasusi, na kiteknolojia ili kuendana na asili ya vitisho vya kisasa.

Nafasi ya Misri haiishii ndani tu, bali inaenea hadi kwenye ngazi za kikanda na Afrika. Misri ina eneo la kijiografia linaloifanya kuwa kitovu kati ya Afrika Kaskazini, Pembe ya Afrika, na eneo la Sahel—maeneo yanayokabiliwa zaidi na shughuli za makundi ya kigaidi kama vile Daesh (ISIS), Al-Qaeda, Boko Haram, na Al-Shabaab. Kutokana na hili, kusaidia uwezo wa nchi za Afrika katika nyanja za mafunzo ya kiusalama, kubadilishana taarifa, na kujenga taasisi madhubuti ni sehemu ya msingi ya usalama wa kitaifa wa Misri, kwa sababu utulivu wa Afrika unaakisi moja kwa moja utulivu wa Misri.

Pia, Cairo ina zana zenye ushawishi wa kidiplomasia ndani ya Umoja wa Afrika, Jumuia ya Madola ya Kiarabu, na Umoja wa Mataifa. Hii inaipa fursa ya kuongoza mipango ya pamoja inayolenga kupambana na ufadhili wa ugaidi, kuimarisha usalama wa mipaka, na kukabiliana na usajili wa vijana mtandaoni, pamoja na kusaidia mipango ya maendeleo katika maeneo dhaifu yanayotumiwa na makundi yenye msimamo mkali.

Ni muhimu pia kwa Misri katika hatua inayofuata kuitikia maono ya mbali zaidi yanayojikita kwenye dhana ya “Usalama wa Kinga” (Preventive Security)—yaani kuzuia kuibuka kwa msimamo mkali kabla haujawa tishio la kiusalama. Hili linafikiwa kupitia uwekezaji kwa vijana, ujasiriamali, elimu ya kidijitali, uchumi wa kijani, na uvumbuzi; Kwani jamii zenye fursa halisi za ukuaji zinakuwa hatarini kidogo kushawishiwa na makundi yenye msimamo mkali.

Katika muktadha huu, Misri inaweza kuongoza mpango wa kiafrika wa kuanzisha Kituo cha Kikanda cha Tahadhari ya Mapema Kuhusu Msimamo mkali na Ugaidi. Kituo hiki kitategemea Akili Bandia na uchanganuzi wa data kubwa ili kufuatilia nyayo zinazotiliwa shaka, kuangalia mbinu za usajili mtandaoni, na kubadilishana taarifa kati ya nchi za Afrika kwa haraka na kwa ufanisi zaidi. Pia, mipango ya pamoja inaweza kuzinduliwa ili kuwajengea uwezo Maimamu na Wahubiri wa Afrika ndani ya taasisi za kidini za Misri, jambo litakalochangia kueneza mtazamo wa kidini wa wastani barani kote.

Mwelekeo wa kiutamaduni una umuhimu sawa na mwelekeo wa kiusalama. Nguvu laini (Soft Power) ya Misri kupitia vyombo vyake vya habari, sanaa, elimu, vyuo vikuu, na taasisi za kidini ni miongoni mwa zana muhimu zaidi za kupambana na msimamo mkali, kwani inatoa mfano wa kistaarabu unaojikita kwenye msimamo wa wastani, utofauti, na kuwakubali wengine, maadili yanayochangia kujenga jamii zilizoshikamana na tulivu zaidi.

Mustakabali wa mapambano dhidi ya msimamo mkali hautatuliwi kwa silaha pekee, bali kwa uwezo wa mataifa wa kumjenga binadamu, kuimarisha utambulisho wa kitaifa, kufanikisha maendeleo kiujumla, na kudhibiti haki ya kijamii. Katika muktadha huu, Misri ina sifa zote zinazoistahilisha kutoka kuwa nchi iliyofanikiwa kulinda usalama wake wa ndani hadi kuwa nchi inayoongoza juhudi za kikanda na Afrika za kuunda mfano jumuishi wa kupambana na msimamo mkali, mfano unaounganisha usalama, maendeleo, fikra, na diplomasia. Kila mara Misri inapofanikiwa kusambaza mfano huu, ndivyo uwezo wake wa kulinda usalama wake wa kitaifa, kuimarisha nafasi yake ya kikanda, na kuthibitisha nafasi yake kama nguzo ya utulivu na mshirika mkuu katika kujenga mustakabali salama zaidi kwa bara la Afrika na eneo la Kiarabu unavyoongezeka.

اظهر المزيد

موضوعات ذات صلة

زر الذهاب إلى الأعلى