Alarab Language

Biashara ya Ndani ya Afrika: Kutoka Matarajio Hadi Kufikia Maslahi na Ujenzi wa Nchi ya Kitaifa

Rami Zahdi — Makamu wa Rais wa Kituo cha Al-Arab

Biashara ya ndani ya Afrika si wazo la kinadharia linalotajwa tu katika hotuba za mikutano ya kilele au taarifa za mashirika ya kikanda, bali imegeuka kuwa moja ya nguzo za kimsingi za kuelewa mustakabali wa bara na uwezo wake wa kukabiliana na misukosuko inayofuata  iwe ya kiuchumi, kiusalama au kijamii. Bara ambalo lina zaidi ya watu bilioni 1.4, lina takribani asilimia 30 ya akiba ya madini duniani, na linachangia zaidi ya asilimia 60 ya ardhi ya kilimo isiyotumika kimataifa, bado kiwango cha biashara yake ya ndani hakizidi, katika makadirio bora zaidi, asilimia 15 hadi 18 ya jumla ya biashara yake ya nje. Hii ni ikilinganishwa na takribani asilimia 60 ndani ya Umoja wa Ulaya, na zaidi ya asilimia 40 barani Asia.ukosefu huu mkubwa hauoneshi kupunguza kwa rasilimali, bali ni mgogoro wa maono, miundombinu, na usimamizi wa maslahi ya pamoja.

Matarajio ya Afrika ya kuimarisha biashara ya ndani yalijidhihirisha kinadharia kupitia uzinduzi wa Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika (AfCFTA), linalojumuisha nchi 54 zenye jumla ya pato la ndani linalozidi dola trilioni 3.4. Ripoti za Benki ya Dunia zinakadiria kuwa utekelezaji kamili wa makubaliano haya unaweza kuongeza kiwango cha biashara ya ndani kwa zaidi ya asilimia 50 ifikapo mwaka 2035, na kuwaondoa zaidi ya Waafrika milioni 30 kutoka katika umaskini uliokithiri. Hata hivyo, kiwango kati ya kusaini na kutekeleza bado ni mkubwa, una vikwazo vya kimuundo vinavyozidi masuala ya ushuru wa forodha na kuingia katika maeneo ya kina na hatari zaidi.

Kizuizi cha kwanza kinahusiana na udhaifu wa miundombinu ya kuvuka mipaka ambapo takwimu za Benki ya Maendeleo ya Afrika zinaonesha kuwa pengo la ufadhili wa miundombinu barani linakadiriwa kati ya dola bilioni 68 hadi 108 kwa mwaka. Barabara zisizokamilika, bandari zenye ufanisi mdogo, mitandao ya reli iliyogawanyika, pamoja na gharama kubwa za usafirishaji na lojistiki, husababisha bei ya bidhaa za Kiafrika kupanda kwa hadi asilimia 40 ikilinganishwa na bidhaa za kimataifa.

Kizuizi cha pili, kinahusiana na kufanana kwa miundo ya uzalishaji, ambapo nchi nyingi husafirisha malighafi zilezile bila ya kuongeza thamani, jambo linalopunguza fursa za ujumuishaji wa kweli wa kiuchumi na kuimarisha ushindani hasi badala ya ushirikiano wa kimkakati.

Ama kizuizi cha tatu, kinajitokeza katika urasimu na udhaifu wa uratibu wa kitaasisi, ambapo shehena moja ya bidhaa inaweza kupata zaidi ya siku kumi kupitishwa katika baadhi ya mipaka ya Afrika, ikilinganishwa na masaa machache tu katika makundi ya kiuchumi yaliyoendelea.

Lakini lililo hatari zaidi kuliko yote ni kukosekana kwa uhusiano mzuri kati ya biashara ya ndani ya Afrika na dhana ya nchi ya kitaifa. Biashara siyo tu takwimu za kubadilishana bidhaa, bali ni chombo cha kufikia utulivu, kuimarisha utegemeano wa pamoja, na kukabiliana na vyanzo vya misimamo mikali na ugaidi. Pale maslahi ya kiuchumi yanapounganishwa kati ya nchi, minyororo ya ugavi inaposhikamana, na fursa za ajira za kuvuka mipaka zinapoundwa, jamii hupungua uwezekano wa kupenya na mawazo yenye msimamo mikali. Hivyo, usalama hubadilika kutoka katika mtazamo wa kijeshi kwenda katika mkabala wa maendeleo jumuishi.

Tafiti za Umoja wa Mataifa zinaonesha kuwa kila ongezeko la asilimia 1 katika viwango vya ajira hupunguza uwezekano wa kujiingiza katika vurugu zilizopangwa kwa takribani asilimia 2. Huu ni ushahidi wenye uzito mkubwa, hasa katika bara ambalo zaidi ya asilimia 60 ya vijana wake wanakabiliwa na udhaifu mkubwa wa soko la ajira.

Kuimarisha biashara ya ndani ya Afrika pia kunawakilisha fursa halisi ya kukuza mapato ya kitaifa na kupunguza utegemezi uliokithiri kwa masoko ya nje. Nchi za Afrika hutumia kila mwaka zaidi ya dola bilioni 80 kuagiza chakula kutoka nje ya bara, ilhali minyororo ya thamani ya kikanda katika kilimo na viwanda inaweza kuhifadhi sehemu kubwa ya fedha hizi ndani ya uchumi wa kitaifa. Aidha, kuendeleza na kuimarisha viwanda vidogo na vya kati, na kuviunganisha na masoko mapana ya Afrika, kunajenga msingi imara wa utekelezaji wa mipango ya mageuzi ya kiuchumi, na kunazipa serikali uhuru mpana wa kuchukua hatua bila kufungwa na misukosuko ya masoko ya kimataifa au masharti magumu ya ufadhili.

Fursa za ushirikiano wa Afrika katika uwanja huu ni za kweli, lakini zinahitaji mabadiliko kutoka mantiki ya kauli mbiu kwenda maslahi yaliyopimwa kwa uangalifu. Kinachohitajika ni uwekezaji wa pamoja katika miundombinu, uratibu wa sera za viwanda, kurahisisha taratibu za kibiashara, na kuiwezesha sekta binafsi ya Kiafrika kuwa mshirika halisi badala ya mfuasi. Vilevile, kunahitajika jukumu la msingi la nchi zilizo na uzito wa kikanda, hasa Misri, ili kuunganisha kanda za Afrika, kuhamisha uzoefu, na kuunda majukwaa ya lojistiki na biashara yanayohudumia bara zima.

Hatimaye, biashara ya ndani ya Afrika siyo tu njia ya kiuchumi, bali ni mradi wa kiustaarabu unaolenga kuunda upya imani kati ya watu, kuimarisha taasisi za nchi za kitaifa, na kugeuza jiografia kutoka kuwa mzigo wa kihistoria kwenda kuwa faida ya kimkakati. Kati ya matarajio na vikwazo, fursa bado ipo lakini haitawasubiri kwa muda mrefu wale wanaosita kuinyakua.

اظهر المزيد

موضوعات ذات صلة

زر الذهاب إلى الأعلى